Social Icons

Alhamisi, 27 Machi 2014

JUMLA YA MIZINGA 1,400 YA NYUKI YATUNDIKWA NCHINI


Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bi. M. K Tarishi akihutubia wananchi wa wilayani Mlela mkoani Katavi (hawako pichani) katika kilele cha Siku ya taifa ya kutundika mizinga Machi 18, Mwaka huu.
Mlele, Katavi
Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu imewezesha kila mkoa nchini kutundika mizinga 50 katika kuazimisha Siku ya Kutundika Mizinga kitaifa iliyofanyika Machi 18, Mwaka huu.
Akizungumza wilayani hapa, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bi. M.K Tarishi alisema siku hii inaadhimishwa kitaifa katika Msitu wa Mlele Wilaya ya Mlele na mikoa yote Tanzania Bara inaadhimisha katika ngazi ya Mkoa kwa kutundika jumla ya mizinga 1,400 katika sehemu mbalimbali za mikoa husika.
Aliongeza kuwa Mizinga hiyo imekabidhiwa kwa vikundi vya ufugaji nyuki ili iwe ni chachu ya kuendeleza ufugaji Nyuki kwa kutumia mbinu bora za ufugaji Nyuki unaolenga kumfanya mfugaji aweze kufuga kibiashara ambapo atatakiwa kuwa na mizinga yenye makundi ya Nyuki isiyopungua 30 ambayo ndiyo yenye tija kibiashara.
Alisisitiza kuwa ufugaji wa kibiashara unamfanya mfugaji aweze kuzalisha kiasi cha kilo 450 kwa msimu chenye thamani ya Tshs. 1,500,000 na nta kilo 30 ambazo zina thamani ya Tshs. 150,000 ambayo ni mara mbili na nusu kwa wastani wa pato la mtazania.
Tathimini ya Siku ya Kutundika Mizinga mwaka jana inaonesha kuongezeka mwitikio wa jamii katika Ufugaji Nyuki. Uzalishaji wa asali umeongezeka kutoka tani 9,800 za asali na nta tani 625 kwa mwaka 2012/2013 hadi tani 19,000 za asali na tani 1,200 za nta kwa mwaka 2013/2014.
“Thamani ya kiasi hicho cha uzalishaji katika ngazi ya mfugaji ni sawa na billion 66.5. Lengo ni kuongeza uzalishaji kwa asilimia 50 kwa mwaka katika kipindi cha miaka mitano ijayo,” Alisema Bi. Tarishi.
Wakati huo huo, Wakala wa Huduma za Misitu imeanzisha mkakati wa uzalishaji wa makundi kwa kutumia uzalishaji wa malkia ili kuhakikisha mizinga inakuwa na Nyuki badala ya kusubiria makundi yaingie yenyewe kwenye mzinga.
Akielezea kuhusu Mkakati huo, Bi. Tarishi alisema Mafunzo ya uzalishaji wa malkia na usimamzi wa makundi ya nyuki yalianza tokea mwaka 2013 yakishirikisha wataalamu 47 kutoka Kanda saba za Wakala na wafugaji nyuki 10 ambao walifanya mafunzo hayo kwa vitendo.
Alisema jumla ya malkia 120 wamezalishwa kwa kipindi cha miaka miwili cha mafunzo kwa lengo la kusambaza elimu hiyo ya uzalishaji wa malkia nchini.

Hata hivyo, alisema pamoja na ongezeko hilo uzalishaji bado ni mdogo (14%) ukilinganisha na uwezo wa nchi yetu wa kuzalisha tani 138,000 za asali na tani 9,200 za nta kwa mwaka. 
Aliongeza kuwa katika kuboresha tasnia ya ufugaji nyuki ni kuwawezesha wafugaji kuwa na umoja wao ili kurahisisha huduma za ughani, kukabiliana na changamoto za masoko na kudhibiti ubora wa mazao ya nyuki.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Dkt Rajabu Rutengwe alisema mkoa wake utahakikisha katika kila halmashauri ya mkoa kunakuwa na kituo cha kukusanyia asali ili kuweza kuthibiti ubora wa asali kwa kupima asali hiyo.
“Nimeshaagiza kila halamashauri kuhakikisha imetenga bajeti ya kuanzisha kituo cha kukusanyia asali ili kuweza kupata asali bora na uhakika wa soko kwa wafugaji nyuki, utekelezaji wa suala hili utaanza mara moja katika mwaka ujao wa fedha katika kuhakikisha wananchi wa Katavi wanajiongezea kipato, lishe, dawa na kuhifadhi mazingira,” alisema Dkt. Rutengwe.

Kaulimbiu ya siku ya taifa ya kutundika mizinga mwaka huu ni ilikuwa “BORESHA UFUGAJI NYUKI LINDA UBORA WA MAZAO YAKE”. Kauli mbiu iliyoenda pamoja na MKUKUTA II unaosisitiza kuondoa umasikini kwa wananchi na kuchangia katika pato la Taifa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni